Mimi nimeamua kujitoa mhanga kwa ajili ya kuwaokoa vijana wenzangu. Siogopi hata kufa kwa kusema ukweli.
Amina Chifupa.
1981-2007.

Saturday, December 5, 2009

Nimetamani

Nimetamani kusema, leo nitasema yote,
Nataka wenye hekima, wayapime hayo yote,
Wanipe zao tuhuma, penye ujinga nifute,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Nataka towa maoni, sijui atayejali,
Nina machungu moyoni, bora niseme ukweli,
Yanotendeka nchini, yanipa hisia kali,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Tumewaona wakuu, ukweli wakiogopa,
Watwona tuna makuu, maswali wanayakwepa,
Watuweka roho juu, machungu wanayotupa,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Pengine hakuna dira, chombo chaenda mrama,
Wasotumia busara, wanaturudisha nyuma,
Kisa walipewa kura, vyao ndivyo vyote vyema,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Nchi ina utajiri, watu bado masikini,
Lipi sasa lina kheri, lenye faraja moyoni,
Tusome kwenye Zaburi, tusome kwenye Quran?
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Walizotowa ahadi, hawawezi tekeleza,
Ilikuwa makusudi, nasi hatwezi uliza?
Wamejaa ukaidi, tena wenye kuchukiza,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Huduma za kijamii, zaonekana anasa,
Na wao hawasikii, weshachuma zao pesa,
Wamefanya nchi hii, ni shamba lao kabisa,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Nenda hospitalini, huduma zimedorora,
Wagonjwa hulala chini, huduma zisizo bora,
Wa kumlaumu ni nani, ni wao ama wizara?
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Hebu nenda vijijini, uone ilivyo hali,
Wagonjwa wafa njiani, huduma zilivyo mbali,
Uwe na kitu fulani, isiwe mali kauli,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Shule sasa si masomo, kumepatwa dudu gani?
Kila siku ni migomo, twajenga taifa gani?
Kwenye viti waliomo, vichwani wawaza nini?
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Inavuja mitihani, bado hatufanyi kitu,
Elimu kipimo gani, naona si malikitu,
Wal'opo madarakani, waj'ona miungu watu,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Madai yao walimu, mwataka kwanza agua,
Mwaona siyo muhimu, ni lipi mnalojua?
Twahitaji kufahamu, hili linatusumbua,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Hii kitu ufisadi, yawapeni raha gani?
Rushwa ndo zenu juhudi, taifa li hali gani?
Zi wapi zenu stadi, usia upo kapuni?
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Mnayo raha moyoni, japo taifa lalia,
Mu vipofu hamuoni, mambo yamewanogea,
Hata mwenu akilini, hamwezi kufikiria,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Natamani ningeweza, kutoa kwenu hukumu,
Tena ningetekeleza, hata mkinishutumu,
Maana mwatumaliza, kwa kufanya hali ngumu,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Hukumu kwenu ninayo, wala si mbali mwakani,
Kura yangu nipigayo, iwe mkuki moyoni,
Si maneno nisemayo, bali kura mkononi,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Tokeni usingizini, nawaambia wenzangu,
Tuamue kwa makini, kwa uweza wake Mungu,
Isiwe kama zamani, tumeshachoka machungu,
Nimetamani kusema, wacha niyaseme haya.

Nimesema ya kusema, waungwana kusikia,
Nilosema nimepima, ni kwenu kukadiria,
T'wamue yetu hatima, tumechoka kuumia,
Nimetamani kusema, wacheni nimeshasema.

Tuesday, December 1, 2009

Muda wetu

Fikara bado kuisha, suluhisho kufikia,
Azma kuifanikisha, kwa hatua kuchukua,
Hali hii inachosha, tuiambie dunia,
Tutumie muda wetu.

Sauti iwafikie, wote huko nako kule,
Mbiu wakaisikie, ili wasikose shule,
Balaa waj'epushie, kwa makini wasilale,
Tutumie muda wetu.

Toka thema'ni na tatu, tuligundua nchini,
Kwamba miongoni mwetu, hakuna kinga mwilini,
Iliwashitua watu, hatutaki rudi chini,
Tutumie muda wetu.

Sote tuelimishane, pasipo kuona haya,
Kisha tusaidiane, tusianguke pabaya,
Na mikono tushikane, tukaishinde miwaya,
Tutumie muda wetu.

Tutulie kwenye ndoa, kuyaepuka majanga,
Tusijitie madoa, kuendekeza ujinga,
Jamii kuiokoa, hivyo gonjwa kulipinga,
Tutumie muda wetu.

Hatua kuzichukua, ni jambo la kupendeza,
Hatua kwayo hatua, gonjwa kuliteketeza,
Jamii kuiokoa, siha njema kueneza,
Tutumie muda wetu.

Sunday, November 22, 2009

Hongera bwana Given

Salamu nakuletea, rafiki yangu Given,
Neema nakuombea, kheri nyingi duniani,
Mola amekunyo’shea, kukupa matumaini,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Mola amekubarikia, tangu ungali tumboni,
Njia kakufungulia, mapitoyo duniani,
Heshi kukusimamia, daima uwe mwangani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Mke mwema umepewa, chaguo lako moyoni,
Naye heshima katowa, kaleta nuru nyumbani,
Na Mola mkajaliwa, kwa upendo na amani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Kweli Mungu kajalia, tangia mimba tumboni,
Afya kaisimamia, maradhi yawe pembeni,
Siku itapofikia, sote tuzame rahani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Na siku ikafikia, toto kaja duniani,
Mkeo kakuzalia, kwayo kheri na amani,
Kama alivyojalia, muumba wetu Manani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Nasi tunafurahia, twamkaribisha mgeni,
Daima tutamwombea, maishaye duniani,
Vema apate kukua, kwingine awe kifani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Somo ninakupatia, kwa bintiyo wa thamani,
Kwa wema ukamlea, akuwe kwenye imani,
Aishike njema njia, kwenu awe tumaini,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Nasi tunapaswa pia, kutokuketi pembeni,
Bali ni kusaidia, kuilea yake shani,
Apate kufurahia, siku zote maishani,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.

Beti kenda naishia, rafiki toka zamani,
Siachi kukuombea, baraka kwake Manani,
Kheri kwa shemeji pia, ninasema hongereni,
Hongera bwana Given, kwa kumpata mtoto.


Nakupa pongezi nyingi rafiki yangu wa miaka nenda miaka rudi bwana Given Awadh Msigwa na mkeo kwa kubarikiwa kupata mtoto wa kike hapo jana tarehe 21 Novemba 2009. Maneno yoyote hayawezi kuelezea furaha na hisia zangu. Ninamwomba Mwenyezi Mungu awajalie furaha tele na kheri ili muweze kumlea binti yenu kwa uzuri na hali ipendezayo ili maisha yake yajae mafanikio, furaha na amani.
Pamoja sana mkuu, furaha yako furaha yangu pia.
Amina.

Saturday, November 14, 2009

Nasema ahsante sana

Nakushuru sana Mungu, mema umenijalia,
Ewe muumbaji wangu, sifa nakurudishia,
Bariki maisha yangu, uniangazie njia,
Nasema ahsante sana.

Nakushukuru sana mama, kwanza ni kwa kunizaa,
Umenilea kwa wema, kwa nyota inayong'aa,
Nitashukuru daima, umeniwashia taa,
Nasema ahsante sana.

Nakushukuru mwandani, mpenzi wa moyo wangu,
Kwangu unayo thamani, kwani u sehemu yangu,
Daima uwe pembeni, sitoweza peke yangu,
Nasema ahsante sana.

Ndugu nawashukuruni, mnanithamini sana,
Tangu mwangu utotoni, tungali tukipendana,
Ninawapenda moyoni, na mbarikiwe sana,
Nasema ahsante sana.

Nashukuru marafiki, Mungu amenijalia,
Tungali tupo lukuki, pamoja twafurahia,
Kwa raha ama kwa dhiki, ndani ya hii dunia,
Nasema ahsante sana.

Siku niliyozaliwa, ambayo naadhimisha,
Furaha niliyojawa, ninyi mmesababisha,
Kwa umoja tumekuwa, imara kwenye maisha,
Nasema ahsante sana.

Upendo ndiyo silaha, hakika tunapendana,
Upendo una furaha, kweli twafurahiana,
Na hivyo huleta raha, raha kifani hakuna,
Nasema ahsante sana.

Ahsante pasi kipimo, nawashukuruni sana,
Upendo pasi kikomo, ninawapendeni sana,
Furaha tele iwemo, maisha marefu sana,
NASEMA AHSANTE SANA.

Nawashukuruni sana, mara zisizo na idadi kwa upendo wenu muuoneshao kwangu, siku zote. Ninatamani kusema maneno mengi kuonesha wingi wa furaha na shukrani zangu kwenu, lakini maneno hayajitoshelezi. Ninasema, nawashukuruni sana, ninawapenda sana, na ninawaombea furaha na mafanikio daima.
Pamoja sana.

Wednesday, November 11, 2009

Nakupa wewe zawadi

Nimekaa nikawaza, nini unastahili,
Jambo lenye kupendeza, jambo lenye kuhawili,
Vema lenye kueleza, kwazo hisia kamili,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la dhati.

Kila nachofikiria, bado siwezi ridhika,
Kiwezacho kufikia, mapenzi yalotukuka,
Mola alokujalia, yale yasomithilika,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la dhati.

Wanifaa kila hali, niwache niseme mie,
Wanipa pendo la kweli, niache nijisikie,
Kwako natulia tuli, wewe nikufurahie,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la kweli.

Zawadi hii pokea, nakupa kwa moyo wote,
Mi ndo nilokuchagua, sikulala nikupate,
Pendo halitopungua, nifae maisha yote,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la kweli.

Nitakwonyesha upendo, tena kutoka moyoni,
Unipime kwa matendo, si maneno mdomoni,
Ufae wangu mwenendo, nisikujaze huzuni,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la kweli.

Nitakwombea daima, Mola azidi jalia,
Ili panapo uzima, pendo lizidi kukua,
Imara tweze simama, ndani ya hii dunia,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la kweli.

Nakupenda sana mie, maneno hayatatosha,
Mpenzi unisikie, wewe ndiye wanitosha,
Njoo ukanitibie, homa yangu kuishusha,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la dhati.

Watasema sana watu, ni maneno tuu hayo,
Kwako siogopi kitu, kwa maneno wasemayo,
Sikuachi wewe katu, kwa mapenzi unipayo,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la dhati.

Zinatosha beti kenda, wewe ninajivunia,
Sitochoka kukupenda, kwa penzi linalokua,
Kokote nitakokwenda, zawadi ‘takutunzia,
Nakupa wewe zawadi, nayo ni pendo la kweli.

Saturday, November 7, 2009

Pamoja daima

Wakati wote wa raha, raha tele mioyoni,
Wakati wa furaha, mimi nawe furahani,
Wakati nyota ya jaha, yaangaza maishani,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Furahi pamoja nami, tudumishe urafiki,
Langu kamwe sikunyimi, kwa raha ama kwa dhiki,
U sehemu yangu mimi, kukupoteza sitaki,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Maisha yana milima, ni kupanda na kushuka,
Dunia siyo salama, hutokea kuteseka,
Kwangu upate egama, dhoruba ikikufika,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Mawimbi yakikupiga, sikwachi uzame chini,
Ukishikwa nao woga, ningali mwako pembeni,
Sikwachi kwenye mafiga, sikwachi kikaangoni,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Sikubali uanguke, nitakuwa yako nguzo,
Sitaki utaabike, kama ninao uwezo,
Na wala usidhurike, upatwapo matatizo,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Unishike nikushike, tuzidi kuwa imara,
Daima nikukumbuke, nikwepushie madhara,
Nisikuache mpweke, nikuombee nusura,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Nikuonyeshe upendo, wa thamani na kujali,
Si maneno ni matendo, yenye dhamira ya kweli,
Twenende wetu mwendo, pamoja kwa kila hali,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Maisha yanayo siri, hujui lijalo kesho,
Hutokea ujasiri, kukumbwa navyo vitisho,
Kama ilivyo safari, mambo yote yana mwisho,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Rafiki una thamani, siwezi kukupoteza,
Sithubutu abadani, peke kukutelekeza,
Namwomba wetu Manani, an’epushe kuteleza,
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Kaditama namaliza, rafiki ninakupenda,
Sichoki kukueleza, daima nitakulinda,
Nasi tumwombe Muweza, kokote tunakokwenda
Mimi nawe tutakuwa, pamwe daima dawamu.

Monday, November 2, 2009

Uvivu niondokee

Nimekuwa na uvivu, sijui waja na nini,
Mawazo yawa makavu, sinalo jipya kichwani,
Tabia hii ni mbovu, siipendi asilani,
Uvivu niondokee.

Uvivu wa kuandika, mbona unaniandama?
Na sikutaki ondoka, mbona unanisakama,
Na siwezi kukutaka, wewe si rafiki mwema,
Uvivu niondokee.

Wewe ni mtu mbaya, wala usinizowee,
Tena huna hata haya, hebu uniondokee,
Usidhani nakugwaya, na usinitembelee,
Uvivu niondokee.

Wanifanya mi mjinga, tena niso na maana,
Kwako mi umenifunga, na kunitesa kwa sana,
Hadharani nakupinga, sitaki nikwone tena,
Uvivu niondokee.

Mimi si mtumwa wako, unikome ukomae,
Sizitaki nira zako, kwa haraka utambae,
Rudi huko utokako, kuja kwangu ukatae,
Uvivu niondokee.

Leo ninasema wazi, siku hizi 'meniteka,
Kuendelea siwezi, nasema wazi ondoka,
Nataka kufanya kazi, siachi mi kuandika,
Uvivu niondokee.

Nenda kwangu usirudi, asilani abadani,
Niache mi nifaidi, mawazo pevu kichwani,
Na ninatoa ahadi, sikutaki maishani,
Uvivu usirudi tena.

Monday, October 26, 2009

Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru

Ninapiga goti chini, niitoe sala yangu,
Ya dhati toka moyoni, mbele zako ewe Mungu,
Unionaye sirini, na kujua shida zangu,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Nafikiri naumia, nashindwa la kulifanya,
Mambo yaliyotukia, hakika yanachanganya,
Hivyo ninakulilia, kwake ukawe mponya,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Maisha si utabiri, ya kesho tukayajua,
Ni vigumu kubashiri, kitakachotusumbua,
Mambo huenda sifuri, na maradhi kuugua,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Mola wewe mfariji, ufariji moyo wake,
Rafiki yu mhitaji, iangaze njia yake,
Wewe ndiwe mwema jaji, tazama matendo yake,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Mola wewe kiongozi, umuongoze daima,
Chuki dhidiye zi wazi, umjalie uzima,
Aweze ruka viunzi, abaki kuwa salama,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Ewe wetu Maulana, umnusuru rafiki,
Angali shidani sana, umuondolee dhiki,
Rafiki tunapendana, huzuni haipimiki,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Popote alipokosa, Rabana mhurumie,
Wadhalimu wamtesa, ya Karimu umwokoe,
Wanamjengea visa, kilio ukisikie,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Muumba wangu Manani, uzidi kutujalia,
Nina imani moyoni, kwani wewe husikia,
Hutuachi twende chini, ahsante nakupatia,
Rafiki yupo shidani, Mola wangu mnusuru.

Monday, October 19, 2009

Muungwana ni kitendo

Sikuaga ninakiri, nami nikatokomea,
Msione ni kiburi, kuwa kimenizidia,
Aibu hii dhahiri, kweli nimewakosea.

Msamaha naombeni, maana nimekosea,
Nikaingia mitini, kwa heri sikuw'ambia,
Msinitenge kundini, maana nitafulia.

Majambo yamenikumba, nashindwa kusimulia,
Ila mimi nawaomba, ihsani kunifanyia,
Ili nisiweze yumba, nikateswa na dunia.

Dunia kweli ni shule, kwa yanayotutokea,
Uwe huku ama kule, huwezi kuyakimbia,
Yakupasa usilale, maisha kupigania.

Hivyo mie naja kwenu, najua nimekosea,
Sikuwapeni fununu, yapi yamenitokea,
Siyo maji kwenye kinu, ninachohangaikia.

Monday, October 5, 2009

Upweke

Upweke jama adhabu, upweke unasumbua,
Upweke ni maghilibu, kukufanya kuugua,
Watamani wa karibu, nenolo taelijua,
Upweke.

Upweke hutesa sana, umpendaye awe mbali,
Utamuwazia sana, hata mara alfu mbili,
Kwa usiku na mchana, maumivu ni makali,
Upweke.

Upweke unakondesha, chakula hukitamani,
Upweke unahenyesha, simanzi tele moyoni,
Homa pia hupandisha, na mwokozi humuoni,
Upweke.

Upweke tele mateso, hata machozi kulia,
Moyoni ni manyanyaso, nao moyo kuumia,
Wala si kimasomaso, kwani huleta udhia,
Upweke.

Upweke ni kama jela, huleta nyingi simanzi,
Huwezi hata kulala, maisha tele majonzi,
Utapiga hata sala, uruke vyote viunzi,
Upweke.

Upweke sawa na shimo, mtu ukatumbukia,
Nako shimoni uwamo, wateswa nayo dunia,
Kwani hauna makamo, kuweza kuvumilia,
Upweke.

Wednesday, September 30, 2009

Mwisho wa mwezi

Mwisho wa mwezi ni mambo, tena kubwa burudani,
Mfukoni hakujambo, na raha hadi moyoni,
Pesa sabuni ya roho.

Pesa sabuni ya roho, nazo siku zimefika,
Pesa inao uroho, tamaaye kuzishika,
Tamu za mwisho wa mwezi.

Tamu za mwisho wa mwezi, kwani ushazisotea,
Umefanya sana kazi, hakiyo wakikugea,
Ifurahi familia.

Ifurahi familia, rudi nyumbani mapema,
Pesa ikikuzingua, kwenye shimo utazama,
Eti pesa ni shetani.

Eti pesa ni shetani, hasa ukishazipata,
Hulali hata nyumbani, matako kulia mbwata,
Mfalme ndiyo wewe.

Mfalme ndiyo wewe, na kizungu waongea,
Na hadhira usikiwe, na sifa kukutolea,
Huo ndo mwisho wa mwezi.

Huo ndo mwisho wa mwezi, wa mwingi umaridadi,
U chakari hujiwezi, kichwa maji kuzidi,
Akibayo kukauka.

Akibayo kukauka, hujali kuhusu kesho,
Wewe ni wa uhakika,
Mwezi ufikapo mwisho,
Mwisho wa mwezi ni raha.

Saturday, September 26, 2009

Mpenzi rudi hima

Kusubiri nimechoka, na muda wazidi kwenda,
Mwenzio nataabika, mwili wazidi kukonda,
Raha iliniponyoka, wewe mbali umekwenda,
Urudi basi mpenzi, nakungojea kwa hamu.

Nakungojea kwa hamu, siku utakayorudi,
Unipe mashamshamu, kwani u wangu waridi,
Mapenzi yako matamu, nipate kuyafaidi,
Kwani nimekuchagua, mwingine simtamani.

Mwingine simtamani, nd'o maana nakungoja,
U ndani mwangu moyoni, wewe pekee mmoja,
Wewe huna kifani, urudi tuwe pamoja,
Ona nachanganyikiwa, natamani kukuona.

Natamani kukuona, wewe unipaye raha,
Vinginevyo raha sina, nitakosa hata siha,
Juwa nakupenda sana, wewe u yangu furaha,
Mpenzi usikawie, bure nitamwaga chozi.

Bure nitamwaga chozi, kukuona nikikosa,
Peke yangu sijiwezi, penzi lako lanitesa,
Rudi wangu laazizi, unipaye mi' hamasa,
Nangoja leo na kesho, fanya urudi mapema.

Fanya urudi mapema, upweke wanielemea,
Jitahidi fanya hima, urudi kuniokoa,
Nisije kupata homa, na kuzidi kuumia,
Tabibu wangu ni wewe, rudi ili unitibu.

Rudi ili unitibu, maradhi ya moyo wangu,
Maradhi yan'onisibu, ni wewe mpenzi wangu,
Wewe u wangu muhibu, shahidi yangu ni Mungu,
Mpenzi usichelewe, homa itanizidia.

Homa itanizidia, endapo utachelewa,
Hivyo nakusubiria, raha nataka kupewa,
Useme nikasikia, kwamba hima utakuwa,
Umekuja kunitibu, kabla sijatibuka.

Sunday, September 20, 2009

Utu wema

Ndiyo haswa sifa yako,
Iliyo moyoni mwako,
Wema kwa rafiki zako,
Mola amekujalia.

Wema wako wa moyoni,
Ni kitu chenye thamani,
Mwinginewe hafanani,
Hakika najivunia.

Wema wako wenye dhati,
Usiojali wakati,
Wema mwingi kibati,
Yeyote kufurahia.

Roho yenye utajiri,
Nzuri kushinda johari,
Kuwa nawe ni fahari,
Kwa maisha ya dunia.

Umepewa utu wema,
Wenye thamani daima,
Moyo wangu wanituma,
Sifazo kukupatia.

Kwa Mola nakuombea,
Azidi kukupatia,
Heri na fanaka pia,
Katika hii dunia.

Thursday, September 17, 2009

Mola wangu nisamehe

Mola unayenipenda, unipaye afya njema,
Mlinzi ninapokwenda, wanijalia uzima,
Kwa dhambi ninazotenda, unionee huruma,
Mola wangu unisamehe.

Matendo yangu mabaya, tena yenye kuchukiza,
Nitendayo bila haya, wengine kuwaumiza,
Kwa kila lililo baya, na bado nikajikweza,
Mola wangu nisamehe.

Niyatendayo sirini, najidanganya mwenyewe,
Japo watu hawaoni, lakini waona wewe,
Nisipoteze imani, naomba nikombolewe,
Mola wangu nisamehe.

Machafu mawazo yangu, na mengine ya moyoni,
Husuda kwao wenzangu, ugomvi na majirani,
Usin'ache peke yangu, nitaishia njiani,
Mola wangu nisamehe.

Maneno yangu machafu, maneno yenye kuudhi,
Mimi si mkamilifu, sipendi nikose radhi,
Siitaki tena hofu, dhambi isiwe maradhi,
Mola wangu nisamehe.

Mola wangu naja kwako, baraka unijalie,
Niokoe mja wako, dunia 'sinizuzue,
Na utukufu ni wako, Mola wangu nisikie,
Mola wangu nisamehe.

Thursday, September 10, 2009

Usichoke

Maisha ni kama vita, usichoke kupigana,
Hata kama ukigota, endelea kupambana,
Bado muda wa kutweta, bado ni mapema sana,
Usichoke mwanakwetu.

Nenda shule ukasome, uongeze maarifa,
Ukiwa huko jitume, uliinue taifa,
Nenda kakazane shime, utajipatia sifa,
Usichoke mwanakwetu.

Amka wahi kazini, ili uongeze tija,
Ujuzi wako kichwani, taifa linaungoja,
Ujitume ofisini, na wenzako kwa pamoja,
Usichoke mwanakwetu.

Pigana pasi kuchoka, yapiganie maisha,
Jitihada zako weka, ustawi kufanikisha,
Kwa dhamira ya hakika, malengo kufanikisha,
Usichoke mwanakwetu.

Mwiko kukata tamaa, bado ni ndefu safari,
Kurudi nyuma kataa, pambana nazo hatari,
Tumia kila wasaa, maisha kutafakari,
Usichoke mwanakwetu.

Usifanye masikhara, maisha hayendi hivyo,
Kwa hiyo kuwa imara, vile iwezekanavyo,
Nawe utazidi ng'ara, namna itakiwavyo,
Usichoke mwanakwetu.

Friday, September 4, 2009

Huba

Nijaze mie mahaba,
Ili nile nikashiba,
Nipe mapenzi ya huba,
Nitosheke na dunia.

Nipe chakula kitamu,
Kinijaze mi’ wazimu,
Kinipandishe stimu,
Nibaki sikilizia.

Nigee mapenzi yote,
Yaniingie nidate,
Raha kamili nipate,
Raha isiyopungua.

Niambie wanipenda,
Siposema nitakonda,
Hata homa kunipanda,
Moyoni nikaumia.

Nifanye nifurahie,
Katu mi’ nisiumie,
Mapenzi nijivunie,
Na raha kujisikia.

Nipe mimi peke yangu,
Usimpe na mwenzangu,
Umeumbwa uwe wangu,
Mungu amenipatia.

Kunipenda usichoke,
Wanifanya niridhike,
Na moyo uburudike,
U wangu najivunia.

Tuesday, September 1, 2009

Mlevi na Falsafa yake

Kwamba asiyejua,
Na hajui kwamba hajui
Ndiye mwerevu zaidi,
Hapa duniani,
Wataka kushangaa?

Bora asiyejua,
Na anajua kwamba hajui,
Kwani tungesemaje?
Ilhali wengine,
Wametuvisha vidoto!

Wasomi na wanasayansi,
Nd'o walogeuka,
Wamekuwa wanasiasa
Sasa wameshatonoka
Wakukumbuke wewe,
Kwa lipi hasa
Ulilonalo?

Maana ya maneno:
Vidoto - vipande vya nguo maalumu wafungwavyo ngamia machoni wasafiripo jangwani.
Tonoka - kuwa na hali nzuri kwa sababu ya mafanikio fulani.

Wednesday, August 26, 2009

Falsafa ya Mlevi I

Na Dkt. Masangu Matondo Nzuzullima


Walimwengu wanasema:
Kuna kujua
Na kujua kwamba unajua
Pia kuna kujua
Na kutojua kwamba unajua
Lakini pia kuna kutojua
Na kujua kwamba hujui
Pia kuna kutojua
Na kutojua kwamba hujui

Walimwengu pia wanasema:
Mtu anayejua
Na kujua kwamba anajua
Yeye ni mwerevu na msomi
Na mtu anayejua
Lakini hajui kwamba anajua
Yeye ni mdadisi na mgunduzi
Mtu asiyejua
Na anajua kwamba hajui
Yeye ni mwanafunzi
Lakini mtu asiyejua
Na hajui kwamba hajui
Yeye ni mpumbavu!

Mimi mlevi ninasema:
Yote haya ni uwongo na uzushi
Mtu anayejua
Na kujua kwamba anajua
Yeye ni mpumbavu!
Kwani wasomi, wanasayansi na wanasiasa
Hawakugeuka Mashing’weng’we,
Na kutufikisha Pagak?

Mimi mlevi nasisitiza
Mtu pekee mwerevu hapa duniani
Ni mtu asiyejua
Na hajui kwamba hajui!

Maneno Magumu:

Mashing’weng’we - mazimwi yalayo watu katika hadithi za Kisukuma
Pagak - kutoka katika kitabu cha Wimbo wa Lawino kilichoandikwa na Okot p'Bitek. Ni mahali ambako mtu akienda harudi yaani kuzimuni.

(c) Dr. Masangu Matondo Nzuzullima

Ahsante sana Prof. Matondo Nzuzullima kwa shairi hili.

Tuesday, August 25, 2009

Hongera Mubelwa Bandio

Nimeisikia mbiu, alfajiri imelia,
Ili tusijisahau, maisha kupigania,
Ili nasi angalau, mahali tukafikia,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Mwaka sasa umekwisha, unaandika huchoki,
Wajua haya maisha, hujaa mingi mikiki,
Wengine kuelimisha, ni jambo la kirafiki,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Upo kwenye mapambano, ujenzi walo taifa,
Hujalala kama pono, wastahili nyingi sifa,
Washika yetu mikono, ili tuzizibe nyufa,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Mubelwa bado kuchoka, upo kwenye msafara,
Ungali kwenye pilika, kwa zako huru fikra,
Nakuombea baraka, uzidi kuwa imara,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Ingawa ni mwaka 'moja, umefanya kazi nzuri,
Umejenga vema hoja, umetupa kufikiri,
Umedumisha umoja, umetupa umahiri,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Niliwahi kuandika, MZEE WA CHANGAMOTO,
Kutwambia hajachoka, mambo yalo motomoto,
Miziki ya uhakika, yenye midundo mizito,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Nakuombea kwa Mungu, uwe na afya imara,
Kwenye haya malimwengu, akwepushie papara,
Uepushiwe kiwingu, nyota izidi kung'ara,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Mubelwa mwendo ukaze, usiache harakati,
Mawazo uyaeleze, tena kwa kila wakati,
Ili nasi tujifunze, nawe uwe katikati,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Na wanablog wote, siachi kuwapongeza,
Heri nyingi mzipate, Mola atawaongoza,
Mlipo pale popote, mengi sana mwatufunza,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Namaliza kaditama, Mubelwa hongera sana,
Ujaliwe yalo mema, usiku nao mchana,
U rafiki yetu mwema, nasi twakupenda sana,
Nakupa zangu pongezi, kaka Mubelwa Bandio.

Saturday, August 22, 2009

Mola tuongoze

Dunia tambara bovu, wahenga walishanena,
Yataka uvumilivu, na kukuomba Rabana,
Dunia mti mkavu, majaribu mengi sana,
Mola utuongoze.

Dunia hii hadaa, huhadaa ulimwengu,
Hata kwa walo shujaa, huonja yake machungu,
Ulaghai umejaa, kwenye hayo malimwengu,
Mola utuongoze.

Tukiwa sisi pekee, hatutoweza kushinda,
Hivyo utusimamie, mambo yasije kupinda,
Ili mbele twendelee, tuponye vyetu vidonda,
Mola utuongoze.

Tupe mioyo misafi, tusiwe na majivuno,
Tuondolee ulafi, hata panapo vinono,
Imani iwapo safi, twalitimiza agano,
Mola utuongoze.

Twepushie ufitini, majungu tusiabudu,
Tushibe njema imani, tusiwe wala vibudu,
Chuki isiwe myoyoni, wala kupenda ghadhabu,
Mola utuongoze.

Mali zisitulaghai, tukajawa na kiburi,
Tukakwona haufai, tukajawa ufahari,
Tupe yalo anuai, tujifunze kufikiri,
Mola utuongoze.

Mola utuongoze, wewe utusimamie,
Twataka tusiteleze, wewe utupiganie,
Mola utuelekeze, na tukutumainie,
Mola utuongoze.